
Simiyu. Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro ametoa onyo akisema wamejiweka tayari kukabiliana na watu, wakiwemo wanasiasa wanaohamasishana kuandamana nchi nzima kinyume cha sheria.
Sirro alisema hayo jana mjini Bariadi baada ya kukutana na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa wa Simiyu alikokuwa ziarani kukagua utayari wa askari wa jeshi hilo.
“Kuna makundi ya vijana wanaojiita wana mapinduzi wanahamasishana na kupanga kuandamana nchi nzima wakiratibiwa na chama kimoja cha siasa, tumejipanga kuwadhibiti na tutawakamata wote bila kujali vyeo na madaraka yao,” alisema.
Wakati IGP Sirro akitoa onyo hilo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa aliwazungumzia wanaosambaza ujumbe wa kuwahamasisha wananchi kuandamana kwenye mitandao ya kijamii akisema watachukuliwa hatua za kisheria.
Kamanda Mambosasa akizungumza na waandishi wa habari jana, alisema Jeshi la Polisi haliwezi kukubali kuona watu hao wanaiingiza nchi katika matatizo na kusababisha amani kupotea.
“Wananchi msikubali kutumiwa, hawa wanaohamasisha baadaye wanakaa pembeni na kuwaacha mnaingia kwenye matatizo. Watakaojaribu kuandamana tutawakamata na kuwachukulia hatua, hatuwezi kukubali watu wachache kutuvurugia amani ya nchi,” alisema Mambosasa.
Sirro kwa upande wake aliwataka wazazi na walezi kuwaonya na kuwazuia vijana wao kushiriki maandamano yasiyo na kibali kwa sababu hakuna atakayevunja sheria atakayesalimika bila kuchukuliwa hatua stahiki.
“Kuvunja sheria ni jambo rahisi lakini madhara yake ni makubwa. Wananchi wasijiingize kwenye mambo yakiwemo uhalifu ambayo mwishowe huwagharimu,” alisema.
Katika hatua nyingine, Mambosasa alisema polisi inawashikilia watu wawili wakituhumiwa kuhusika na kifo cha aliyekuwa katibu wa Chadema Kata ya Hananasif, Daniel John.
Alisema Februari 23 saa 5:30 usiku eneo la Hananasif, polisi waliwakamata mwanamke na mwanamume wanaodaiwa kuhusika na kifo cha John.
“Tunapoletewa malalamiko lazima tuyafanyie kazi hivyo tulianza uchunguzi juu ya mauaji hayo, hatuwezi kutaja majina kwa kuwa tunaendelea na upelelezi ili kujua mtandao wote,” alisema Kamanda Mambosasa.
Akizungumzia uchunguzi kuhusu kifo cha aliyekuwa mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwilini aliyepigwa risasi Februari 16 wakati polisi wakiwatawanya wafuasi wa Chadema waliokuwa wakiandamana kuelekea ofisi ya msimamizi wa uchaguzi wa ubunge Jimbo la Kinondoni, alisema unafanyika kama ilivyo kwa kesi nyingine.
Kamanda Mambosasa alisema kuuawa kwa mwanafunzi huyo ni matokeo ya maandamano ya wanachama wa Chadema eneo la Mkwajuni.
Alisema polisi pia imemkamata mkazi wa Kinondoni, Rajabu Mohamed (25) maarufu Rajeshi akituhumiwa kuwakamata wanawake, kuwaingiza kwa nguvu kwenye gari lake, kuwapora na kuwafanyia vitendo vya ukatili.
Mambosasa alisema mtuhumiwa alikamatwa Kinondoni akituhumiwa kuwapata wanawake kwa kuwalaghai kuwa yeye ni mfanyabiashara.
Alisema baada ya kuwapora wanawake mtuhumiwa huyo huzunguka nao akiwatisha kwamba yeye ni freemason na ana uwezo wa kuwaua kwa kuwanyonya damu au kuwakata viungo vya miili yao.
“Kupitia vitisho hivyo wanawake walilazimika kutoa neno la siri la simu zao, alichukua kadi zao za benki na kuwaibia fedha kupitia mashine za kutolea fedha (ATM),” alisema Kamanda Mambosasa.
Mtaka asifu usalama Simiyu
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka alisema matukio makubwa ya kihalifu yaliyokuwepo mkoani humo yamepungua.
Alisema licha ya askari kufanya kazi nzuri, ukosefu wa nyumba za kuishi ni changamoto inayosababisha wengi kupanga mitaani, hivyo kuzoeana na raia kiasi cha kuathiri utendaji wao wa kazi.
“Ni vyema kuwa na mpango wa bajeti maalumu kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za polisi mkoani Simiyu,” alisema Mtaka.
Comments
Post a Comment